MTAZAMO WA UISLAMU JUU YA HISTORIA.

Ndugu wasomaji wa blog hii ya isspyetu baada ya kuangalia mtazamo wa wasiokuwa waislamu juu ya historia sasa tuangalie mtazamo wa waislamu juu ya historia





 by Ahmed Mnungamo



 Imeshabainishwa  kuwa  Historia,  kwa  ujumla,  ni  kumbukumbu za  matendo  na  matukio  yanayohusu  maisha  yote  ya  mwanaadamu katika  jamii  yake  kwa  muda  wote  uliopita

Uislamu  unaitizamaje  Historia  ya  mwanaadamu?

Mtizamo  wa Uislamu  juu  ya  historia  kwa  ujumla  unatofautiana  sana  na  ule  wa makafiri.

Ambapo  makafiri  wanadai  kuwa  hapana  Muumba  wa Ulimwengu  na  vyote  vilivyomo  kwa  ujumla,  Uislamu  unauhusisha Ulimwengu  (Universe)  na  vyote  vilivyomo  akiwemo  mwanaadamu, na  Muumba  mmoja  tu  Mwenye  Hekima  na  Ujuzi  usio  na  kikomo, ambaye  ameumba  kila  kitu  kwa  lengo  maalumu.

LENGO LA MAUMBILE YOTE YALIYOMZUNGUKA MWANADAMU.

Mwenyewe Muumba Allah(s.w),  anabainisha  lengo  la  kumbwa mbingu  na  ardhi  na  vyote  vilivyomo  katika  aya  zifuatazo:



هُوَ الَّذِي خَلَقَ لَكُمْ مَا فِي الْأَرْضِ جَمِيعًا ثُمَّ اسْتَوَىٰ إِلَى السَّمَاءِ فَسَوَّاهُنَّ سَبْعَ سَمَاوَاتٍ ۚ وَهُوَ بِكُلِّ شَيْءٍ عَلِيم

 “Yeye  (Allah)  ndiye  aliyekuumbieni  vyote  vilivyomo  katika  ardhi, tena  akakusudia  kuumba  mbingu;  na  akazifanya  mbingu  saba. Naye  ndiye  ajuaye  kila  kitu”  (2:29).

وَلَقَدْ مَكَّنَّاكُمْ فِي الْأَرْضِ وَجَعَلْنَا لَكُمْ فِيهَا مَعَايِشَ ۗ قَلِيلًا مَا تَشْكُرُون
“Na  hakika  tumekumakinisheni  (tumekukalisheni)  katika  ardhi na  tumekuwekeeni  humo  (vitu  vyote)  vinavyohitajia  maisha  yenu. Ni  shukurani  chache  tu  mnayoshukuru”  (7:10).

Kutokana  na  aya  hizi  tunajifunza  kuwa  maumbile  yote  ya ardhini  na  mbinguni(angani)  yaliyomzunguka  mwanaadamu, anayoyaona  na  asiyoyaona,  yote  yako  pale  kwa  ajili  ya  kumtumikia na  kuboresha  maisha  yake.  Ili  kufikia  lengo  hili,  Allah(s.w) amevitiisha  vitu  hivi  kwa  mwanaadamu  kwa  kuviwekea  sheria madhubuti  za  kimaumbile  (natural  laws):


وَسَخَّرَ لَكُمْ مَا فِي السَّمَاوَاتِ وَمَا فِي الْأَرْضِ جَمِيعًا مِنْهُ ۚ إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَآيَاتٍ لِقَوْمٍ يَتَفَكَّرُون
 “Na  amekutiisheni  vilivyomo  mbinguni  na  ardhini,  vyote vimetoka  kwake.”Bila  shaka  katika  haya  zimo  alama  kwa  watu wanaofikiri  (45:13).

 Kisha,  mwanaadamu  akatunukiwa  akili  na  vipawa  vya  fahamu na  elimu  ya  kumuwezesha  kuyatumikisha  maumbile  kwa  ajili  ya kuboresha  maisha  yake.  Sayansi  na  teknoloia  ni  katika  jitihada  za harakati  za  mwanaadamu  za  kuyatumikisha  maumbile  na  nguvu asili  kwa  ajili  ya  kuboresha  maisha  yake.

LENGO LA MAISHA YA MWANADAMU HAPA ULIMWENGUNI

Kama  vitu  vyote  vimeumbwa  kwa  lengo  la  kumtumikia mwanaadamu,  je,  mwanaadamu  ameumbwa kumtumikia  nani?
Je, lengo  la  maisha  ni  kujipatia  tu  mahitaji  muhimu  ya  maisha  chakula,  nguo  na  makazi?  Mbona  wanyama  nao  wanajitosheleza kwa  mahitaji  hayo  hayo  pamoja  na  kuwa  hawakutunukiwa  kipawa cha  elimu  (kujielemisha)  kama  mwanaadamu?

Je,  ni  busara kukubaliana  na  makafiri  kuwa  lengo  la  maisha  ya  mwanadamu  ni lile  la  kutosheleza  tu  matashi  yake  ya  kinyama?

 Hii  ni  dhana  tu  ya makafiri  kama  Allah(s.w)  anavyotutanabahisha:

وَمَا خَلَقْنَا السَّمَاءَ وَالْأَرْضَ وَمَا بَيْنَهُمَا بَاطِلًا ۚ ذَٰلِكَ ظَنُّ الَّذِينَ كَفَرُوا ۚ فَوَيْلٌ لِلَّذِينَ كَفَرُوا مِنَ النَّار

“Na  hatukuumba  mbingu  na  ardhi  na  vilivyomo  ndani  yake  bure. Hii  ni  dhana  ya  wale  waliokufuru.  Basi  adhabu  kali  ya  moto itawathubutikia  wale  waliokufuru”  (38:27).

Bila  shaka  kwa  wale  wenye  akili  na  busara  wanayakini  kuwa mwanaadamu  hakuumbwa  tu  bure  na  kuletwa  hapa  duniani  bila  ya lengo  lolote  analotarajiwa  na  muumba  wake  alifikie.

Bila  shaka mwanaadamu  atakuwa  na  lengo  la  juu  zaidi  kuliko  viumbe wengine,  hasa  kutokana  na  vipawa  vya  akili  na  elimu alivyotunukiwa  kuliko  viumbe  wengine.

 Lengo  la  kuumbwa mwanaadamu  amelibainisha  Muumba  mwenyewe:

وَمَا خَلَقْتُ الْجِنَّ وَالْإِنْسَ إِلَّا لِيَعْبُدُون

 “Sikuwaumba  majini  na  watu  ila  tu  wapate  kuniabudu”  (51:56).

Maana  ya  Ibada  ni  kumtumikia  Allah(s.w)  katika  maisha  yetu yote.

  Kumtumikia  Allah(s.w)  ni  kumfanya  Allah(s.w)  kuwa  ndiye Bwana  (Rabb)  wetu  pekee  ambaye  ndiye  pekee  tunayepaswa kumtii  kwa  unyenyekevu  kwa  kufuata  barabara  mwongozo  wa maisha  aliyotuwekea.

Utiifu  na  unyenyekevu  wetu  kwa  Allah(s.w) utadhihiri  pale  tutakapopania  kwa  moyo  mkunjufu  kutenda  yale yote  aliyotuamrisha  na  anayoyaridhia  na  kujiepusha  mbali  kutenda yale  yote  aliyotukataza  na  yanayomchukiza  katika  kuendea harakati  za  maisha  yetu  yote  ya  kila  siku.

 Ibada  kwa  mtizamo  huu inamuhusu  kila  mtu  binafsi  na  jamii  kwa  ujumla.  Ili  kila  mtu amuabudu  Allah(s.w)  inavyostahiki,  jamii  inawajibika  kuweka mazingira  ya  kumuabudu  Allah(s.w)  katika  kila  kipengele  cha maisha  kwa  muda  wote  kwa  kuunda  dola  yenye  mamlaka  kamili  ya kuamrisha  mema  yanayoleta  furaha  na  amani  katika  jamii  na kukataza  na  kuyatokomeza  maovu  yanayoleta  huzuni  na  vurugu katika  jamii.

No comments:

Post a Comment