UTANGULIZI
By ahmed mnungamo
Shukurani zote njema zinamstahiki Allah(s.w) aliye Bwana na Mlezi wa walimwengu wote. Rehema na Amani ziwaendee Mitume wake wote pamoja na wale wanaofuata mwenendo wao katika kuhuisha Uislamu katika jamii.
Lengo la kuumbwa watu na kuletwa hapa ulimwenguni ni kumuabudu Mola wao, Allah (s.w), kama inavyobainishwa katika Qur-an:
وَمَا خَلَقْتُ الْجِنَّ وَالْإِنْسَ إِلَّا لِيَعْبُدُون
"Sikuwaumba majini na watu ila wapate kuniabudu". (51:56)
Kumuabudu Allah (s.w) kama lengo la maisha ni kumtii Allah (s.w) kwa unyenyekevu katika kila kipengele na kila nukta ya maisha ya mtu akiwa binafsi na akiwa katika jamii.
Ili watu waweze kumuabudu Mola wao katika kila kipengele na kila nukta ya maisha yao, hawanabudi kwanza, kuwa waumini wa kweli wa Allah (s.w) na kisha kufanya juhudi za makusudi za kuwa makhalifa wa Allah katika jamii.
Makhalifa wa Allah ni wale wanaoiongoza jamii kwa kufuata mwongozo wa Allah (s.w) kupitia kwa Mitume yake na vitabu vyake. Waumini wakifanya jitihada za kusimamisha ukhalifa katika jamii, Allah (s.w) ata wawezesha kufikia lengo la kuumbwa kwao kama anavyoahidi:
وَعَدَ اللَّهُ الَّذِينَ آمَنُوا مِنْكُمْ وَعَمِلُوا الصَّالِحَاتِ لَيَسْتَخْلِفَنَّهُمْ فِي الْأَرْضِ كَمَا اسْتَخْلَفَ الَّذِينَ مِنْ قَبْلِهِمْ وَلَيُمَكِّنَنَّ لَهُمْ دِينَهُمُ الَّذِي ارْتَضَىٰ لَهُمْ وَلَيُبَدِّلَنَّهُمْ مِنْ بَعْدِ خَوْفِهِمْ أَمْنًا ۚ يَعْبُدُونَنِي لَا يُشْرِكُونَ بِي شَيْئًا ۚ وَمَنْ كَفَرَ بَعْدَ ذَٰلِكَ فَأُولَٰئِكَ هُمُ الْفَاسِقُون
"Mwenyezi Mungu amewaahidi wale walioamini miongoni mwenu na kufanya vitendo vizuri, kuwa atawafanya makhalifa katika ardhi kama alivyo wafanya makhalifa wale waliokuwako kabla yao, na kwa yakini atawasimamishia Dini yao Aliyowapendelea, na atawabadilishia amani baada ya khofu yao. Wawe wananiabudu, hawanishirikishi na chochote. Na watakaokufuru baada ya hayo, basi hao ndio wavunjao amri zetu." (24:55)
Lengo la kuletwa Mtume wa mwisho, Muhammad(s.a.w),nalo linabainishwa katika aya ifuatayo:
هُوَ الَّذِي أَرْسَلَ رَسُولَهُ بِالْهُدَىٰ وَدِينِ الْحَقِّ لِيُظْهِرَهُ عَلَى الدِّينِ كُلِّهِ وَلَوْ كَرِهَ الْمُشْرِكُون
"Yeye(Allah) ndiye aliyemtuma Mtume wake(Muhammad) kwa uongofu na kwa dini ya haki ili kuifanya iwe juu ya dini zote (itawale katika jamii) ijapokuwa washirikina watachukia." (9:33,61:9)
Makala hii imekusudiwa kuwaonesha waumini, kwa kurejea historia, uwezekanao wa kutekeleza dhima hii kuu ya kuutawalisha Uislamu katika jamii. Ili kuwafikisha wasomaji kwenye lengo tarajiwa, Makala hii ya "Historia ," kuanzia Mtume Adam(a.s)mpaka hivi leo, imewasilisha maudhui yake kwa anuani ya mada kuu zifuatazo:
1. Dhana juu ya Historia.
2. Historia ya Uislamu kabla ya Muhammad(s.a.w).
3. Historia ya Uislamu wakati wa Muhammad(s.a.w).
4. Ungozi wa Dola ya Kiislamu wakati wa Makhalifa wa Mtume(s.a.w).
5. Kuhuisha Uislamu wakati wa Tabiin.
6. Kuhuisha Uislamu wakati wa Tabiin Tabiin.
7. Kuhuisha Uislamu katika karne ya 20 A.D.
8. Historia ya kuhuisha Uislamu Tanzania.
NB:
Pia katika makala hii tutakazimika kuelezea matukio
mengine ya kihistoria ambayo yataendana na hali na muda kwa kueleza ili liweze kufahamika na kuwafanya wapenzi wasomaji wa page hii kuendana na wakati.
No comments:
Post a Comment